Habari
INDIA KUTOA FURSA ZA UFADHILI WA MASOMO KWA WAHITIMU WA CFR
Balozi wa India nchini, Mheshimiwa Bishwadip Dey, amefanya ziara rasmi katika Kituo cha Uhusiano wa Kimataifa cha Dkt.Salim Ahmed Salim(CFR) Dar es salaam, kwa lengo la kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia kati ya India na Tanzania, hususan katika sekta ya elimu.
Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Balozi amezindua rasmi “Indian Corner” ndani ya maktaba ya Kituo cha Uhusiano wa Kimataifa cha Dkt Salim Ahmed Salim. Uzinduzi huo unalenga kuwawezesha wanafunzi na wadau mbalimbali kupata fursa ya kujifunza zaidi kuhusu India katika masuala ya diplomasia , maendeleo ya kisayansi na teknolojia ,utamaduni na Sera za mambo ya nje za India.Hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za kukuza uelewa wa kimataifa na kuimarisha ushirikiano wa kielimu kati ya mataifa hayo mawili.
Aidha, Balozi Dey alitangaza rasmi fursa za ufadhili wa masomo (scholarships) kwa wanafunzi wanaohitimu masomo yao katika Kituo cha Uhusiano wa Kimataifa, ili kwenda kuendelea na masomo nchini India katika kozi mbalimbali kama taaluma ya akili mnemba(artificial intelligence-AI),masuala ya diplomasia,teknolojia ya sayansi,maendeleo ya uchumi,fursa hizo zinalenga kuwajengea uwezo wanafunzi na kuwaandaa kuwa wataalamu wenye ushindani katika soko la ajira la kimataifa.
Ziara ya Mheshimiwa Balozi Bishwadip Dey ni ishara ya kuendelea kuimarika kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya India na Tanzania, hasa katika kukuza sekta ya elimu, utafiti na ubadilishanaji wa maarifa.
